Jumanne, 1 Aprili 2014

ULAWITI, UBAKAJI WATISHIA TAIFA

Kumefanyika harakati nyingi za kukomesha vitendo hivi, hata hivyo bado vinaendelea.

Ilikuwa ni  saa moja na nusu jioni siku ya jumapili wakati,  Anaheri (siyo jina lake halisi) alipokuwa akitoka dukani alikotumwa na mama yake. Si yeye wala mama yake waliokuwa na wasiwasi wowote, kwani mara kadhaa amekuwa akitumwa nyakati hizo.

Lakini kama balaa linavyoweza kushtukiza, siku hiyo Anaheri, alikamatwa na wanaume wawili waliokuwa wamejificha kichakani. Wakamziba mdomo na kumwingilia. Hawakuishia hapo, waliamua kumvunja shingo na kumuua  binti huyo mwenye miaka 11 tu.

Hii ndiyo hali halisi nchini, ubakaji na ulawiti vimeshika kasi kiasi cha kutishia amani, utulivu na uhuru.

Takwimu za Kitaifa za makosa ya unyanyasaji wa kijinsia kwa mwaka 2012 zinaonyesha wanawake  5745 walibakwa kwa mwaka. Kati yao wanawake wenye umri wa miaka 19 na kuendelea walikuwa 5389 na watoto wenye umri wa chini ya miaka 18 walikuwa 356.

Makosa hayo hayakuishia hapo kwani wanaume na wanawake pia waliendelea kulawitiwa, kwa mwaka 2012 pekee wanaume  691 walilawitiwa. Kati yao,  wanaume waliolawitiwa wenye umri wa zaidi ya miaka 18 ni 456 na watoto ni 235.

Wanawake pia hawakuachwa kwani  kwa mwaka huo huo,  wanawake 35 walilawitiwa  ambao walikuwa na umri wa miaka 19 na kuendelea wakati watoto waliolawitiwa walikuwa ni 11.

Vilevile mauaji ya vikongwe yaliendelea kwa kasi kubwa, kwa mwaka 2012, vikongwe 629 waliuawa. Kati ya hao, wanawake walikuwa  402 na wanaume 227.

Waziri wa  Maendeleo ya Jamii, Jnsia na Watoto, Sophia Simba anasema kazi kubwa ambayo wizara ilifanya ni kuunda sheria kali kuwaadhibu wabakaji na walawiti.

“Kwa jambo hili la kuunda sheria nafikiri tumefanikiwa kwa sababu adhabu ya miaka 30 si ndogo, lakini tunahitaji wanajamii washiriki kuzuia ubakaji,” anasema.

Waziri Simba pia anawataka waandishi wa habari kufanya kazi ya ziada ili kuripoti kuhusu ubakaji kwa kuandika, kufanya utafiti na kuhamasisha.

Naibu Kamishna Mkuu wa Polisi, Adolphina Chialo anasema  unyanyasaji bado ni tishio kwa Watanzania  licha ya juhudi kufanyika kila siku kuwachukulia hatua wanaofanya uhalifu huo.
Chialo anasema  matukio ambayo huripotiwa ndiyo yaliyowekwa kwenye takwimu, hivyo kuna uwezekano kuwa yapo matukio ambayo hayaripotiwi.

“Zamani kesi kama hizi zilikuwa zinaripotiwa chumba cha mashtaka polisi, lakini tuliamua kuanzisha Dawati la Jinsia kwa ajili ya usiri wake. Dawati hili linapokea malalamiko kutoka kwa wanaume, wanawake  na watoto. Tunaposema jinsia hatumaanishi ni wanawake pekee,” anasema

 Anasema unyanyasaji wa aina zote upo na kuongeza kuwa hapo zamani wanawake pekee ndiyo walioonekana kunyanyasika lakini hivi sasa,  hata wanaume wananyanyasika.

Kwa mfano, wapo wanaume ambao wananyanyaswa na wake zao lakini si kwa kupigwa au kubakwa bali matusi na kunyimwa baadhi ya huduma hasa kipato kinaposhuka.

“Wanaume wanafika hapa, wanaeleza manyanyaso  yao wanayoyapata kutoka kwa wake zao na hatua zinachukuliwa. Kwa mfano mawasiliano, kupikiwa, ” anasema.

 Anasema suala kubwa zaidi ni ubakaji na vipigo ambapo vipigo vinahusisha watoto kuchomwa moto na kutukanwa.

“Sasa hivi haya matukio yanaonekana kuwa mengi kwa sababu yanaripotiwa. Zamani  watu walikuwa wanayaficha au wanadhani hakuna pa kuripoti lakini sasa hivi wamejua kuwa kuna suluhisho,” anasema.

 Anasema mikoa ambayo ilidhaniwa kuwa ingekuwa na matukio mengi ya ubakaji, kama Mwanza na Kagera haina matukio mengi kwa sababu ya mila zinazowazunguka.

 Kwa mfano, Wilaya ya Kinondoni, mikoa ya Mbeya na Morogoro  ilikuwa na  matukio mengi zaidi ya ubakaji kuliko Kagera, Mwanza au Tarime jambo ambalo Kamishna Chialo anasema linasababishwa na mila. Kinondoni ina matukio 414 ya ubakaji.

“Kwa mfano Mwanza, kuna hii mila ya Chagulaga, kwao mwanamke hawezi kuripoti kwa sababu kwao ni sehemu ya mila. Lakini kwa sababu ya elimu baadhi ya mikoa imeamka na wanaripoti,” anasema.


Anasema unyanyasaji wa kipigo na mashambulizi pia hauripotiwi kwenye baadhi ya maeneo kwa sababu ya mila. Kwa baadhi ya mila ni haki na sheria kwa mwanamke kupigwa na mume wake.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni