Jumanne, 1 Aprili 2014

TUNA SAFARI NDEFU KATIKA KUCHOCHEA MABADILIKO, KULETA USAWA WA KIJINSIA





Na Hawra Shamte,Mwananchi

Kwanza niwape pongezi wanawake wote duniani kwa kuadhimisha siku yao.
Pili napenda nitumie nafasi hii kuangalia hali ya wanawake tabaan katika maeneo mbalimbali duniani.

Wanawake wanapewa kipaumbele katika mipango ya maendeleo katika nchi nyingi kwa sababu moja kuu; kwa kuwa wao ndiyo waathirika wakuu wa madhila, vita na kila balaa linalotokea duniani.

Tuangalie wanawake wanaotaabika katika maeneo yenye migogoro kama vile Syria na Jamhuri ya Afrika ya Kati. Wanawake ndiyo wanaohangaika na watoto, ndiyo wanaoathirika na vitendo vya ubakaji na unyanyasaji mwingine wa kijinsia.

Wanawake ndiyo wanaochukua jukumu la kuhudumia familia takriban kwa nyakati zote. Wakati mwanamume anaweza kujibaraguza kama nyumbani hakuna chakula, mwanamke atagangamala kuhakikisha chakula kinapatikana kwa ajili ya watoto wake. Atauza vitumbua/maandazi, atatembeza ndizi na mihogo mibichi mitaani, atakopesha khanga, viatu na madira, atalima na atatumika nyumbani kwa watu ili angalau apate vijisenti kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya familia yake.

Kimaumbile mwanamke ni mtu wa amani na utulivu, katika mazingara ya fujo, ugomvi na vita. Utu wa mwanamke huwa uko shakani, hana uhakika wa mustakabali wa maisha ya familia yake. Mwanamke kama mwamvuli, yuko radhi yeye aloe kwa kuihifadhi familia yake.

Wakati wanaume wako ‘bize’ kupigania madaraka, wanawake wameshughulika kulea/kukuza vijana wao. Wangependa watoto wao wawe na maisha bora, watoto wao wapate elimu yenye manufaa, watoto wao wawe na afya njema, watoto wao wale, wacheze, wakue na waishi wakiwa na furaha.

Mutribu mmoja alielezea maisha ya mshumaa akasema kuwa ‘unawaka na kuteketea, kufurahisha umati,’ hali hiyo kwa kiasi kikubwa inaakisi tabia ya mwanamke, kila mara hufikiria furaha ya wengine kabla ya kufikiria furaha yake.

Ni kwa mintarafu hiyo, ndiyo yakawepo maadhimisho ya siku ya wanawake duniani, kwa sababu angalau dunia ipate nafasi ya kutafakari umuhimu, masilahi na fursa za kiumbe huyu aliye na sifa lukuki lakini wenye nguvu hawampi fursa ya kuonyesha vipaji vyake.

Fursa anazonyimwa mwanamke ni nyingi na zinatofautiana kutoka jamii moja hadi nyingine. Zipo jamii zinazomnyima mwanamke fursa ya kupata elimu, zipo zinazomnyima fursa ya kufanya kazi, wapo wasiompa mwanamke nafasi ya kuongoza, wapo pia wanaomwona mwanamke kama kitu cha kuwastarehesha na kuwatimizia mshawasha wao wa matamanio ya mwili na kisha kumdharau kwa kumtupa kama ‘karatasi ya chooni.’

Sheria, imani za kidini na hata mila na desturi nyingi duniani huthamini zaidi wanaume kuliko wanawake. Ziko jamii ambazo ilikuwa akizaliwa mtoto wa kike ndani ya nyumba huchukuliwa na kuzikwa akiwa angali hai. Ziko jamii ambazo ilikuwa mume akifariki dunia, huzikwa pamoja na mke wake aliye hai.
Ziko jamii ambazo hadi leo baba na mama wakitambua tu kuwa mtoto aliyeko tumboni ni wa kike, huhiari kuitoa mimba kabla haijazaliwa.

Ilimradi orodha ya madhila na manyanyaso kwa wanawake ni mengi. Lakini pamoja na matatizo hayo yote ya kijamii, ya kisiasa na hata ya kiitikadi, je, mwanamke mwenyewe anajitambua? Hapo ndipo tunapopaswa kupang’ang’ania.
Mwanamke anapaswa atambue utu wake na nafasi yake katika jamii, kwamba yeye ni binadamu sawa na mwanamume na mwenye haki sawa na mwanamume kimazingira/kijamii na siyo kimaumbile. Hivyo mwanamke anapaswa ahakikishe anaipata nafasi hiyo katika jamii yake.

Wakati pale mwanamume haki zake anapozikuta kwenye sahani ya fedha, mwanamke analazimika azipiganie, ndiyo maana zinatokea dhana za ushirikishwaji na uwezeshwaji kwa sababu kwa kiasi kikubwa hatamu za dola na mamlaka zimeshikwa na wanaume.

Kwa karne tatu sasa, wanawake wamekuwa wakipigania haki zao na nafasi zao katika jamii, toka karne ya 19, mwaka 1908 wakati wafanyakazi wanawake wa nchini Marekani walipoandamana kupinga uonevu waliokuwa wakifanyiwa na waajiri wao, lakini mpaka leo unyanyasaji wa wanawake bado ni tatizo kubwa katika jamii nyingi.

Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Koffi Annan aliwahi kusema: “Ukatili dhidi ya wanawake unasababisha simanzi isiyoelezeka, huumiza familia kutoka kizazi kimoja hadi kingine na kushusha kiwango cha maisha ya familia. Ukatili huo husababisha wanawake washindwe kufikia viwango vya juu vya utendaji wao, unadhibiti ukuaji wa uchumi na kudumaza maendeleo.”

Kaulimbiu ya mwaka huu ni ‘Chochea mabadiliko, kuleta usawa wa kijinsia,’ bila shaka mabadiliko haya yanapaswa kuchochewa kuanzia ngazi ya familia, jamii hadi taifa na anayepaswa kuchochea mabadiliko haya ni mimi na wewe.
Iliniduwaza kidogo wiki iliyopita wakati wa mjadala wa kanuni za Bunge Maalumu la Katiba, wakati walipokuwa wakijadili nafasi za uongozi katika Bunge hilo kwa mtazamo wa kijinsia.

Tuliona jinsi wanaume walivyokuja juu lilipokuja wazo, ikiwa Mwenyekiti atakuwa mwanamume, Makamu Mwenyekiti awe mwanamke, kusema kweli walilipinga wazo hilo kwa hoja za ajabu kabisa.

Waliolitoa wazo lile hawakukusudia kutaka upendeleo, bali walitaka hali ya usawa wa kijinsia izingatiwe katika kuongoza Bunge hilo Maalumu na uzingatifu huo usiwe kwa misingi ya upendeleo wa wanawake tu, bali fursa wapewe wanawake wenye uwezo wa kuongoza.

Hali ile ilitudhihirishia kuwa tutaendelea kupiga kelele za jinsia kwa muda mrefu na pengine kwa karne nyingi zaidi kabla hatujafikia hatua maridhawa, hatua ya kumwona mwanamke kama kiumbe mwenye uwezo sawa na mara nyingine mkubwa zaidi ya mwanamume na kumpa nafasi ya kuonyesha uwezo wake.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni