Ijumaa, 2 Mei 2014

WLAC WATOA MSAADA WA KISHERIA NDANI YA KIJIJI CHA MAISHA PLUS

Baadhi ya Washirka wa Maisha Plus 2014 wakitoa mawazo yao katika semina hiyo

Washiriki wa Maisha Plus 2014 wakipewa vijitabu vinavyohusu sheria mbalimbali 

Washiriki wa Maisha Plus wakifuatilia maelezo toka kwa wanasheria (hawapo pichani)

Moja ya kundi toka kwa washiriki wa Maisha Plus wakifanya mjadala 

Mwanasheria toka shirika la Msaada wa Kisheria kwa Wanawake, WLAC
Ikiwa ni siku ya tatu toka Mama Shujaa wa chakula waingie kijijini Maisha Plus na siku ya 37 toka mashindano hayo yaanze rasmi, jopo la Wanasheria kutoka shirika lisilo la kiserikali la WLAC juzi lilitua kijijini hapo kwa ajili ya kutoa mafunzo mbalimbali ya kisheria kwa wanakijiji hao.

Wanasheria hao ambao ni Faudhia Yasin, Sarah Mambea na Juvenile Rwegasira walianza kwa kuwagawa washiriki katika makundi matatu na kisha kuwataka wajadili visa walivyopewa.

Visa hivi vitatu vililenga kupata ufahamu wa wanakijiji juu ya mambo yanayohusiana na Mjane na urithi, sheria ya ndoa na talaka pamoja na ukatili dhidi ya wanawake.

Makundi yawasilisha visa
Kundi la kwanza liliwakilishwa na washiriki Mbonimpaye Nkoronko kutoka Mtwara, Boniphace Meng’anyi kutoka Dar es salaam na Ngabonziza Daniel kutoka nchini Rwanda. Vijana hawa katika kisa chao waligundua kwamba mtu akishakuwa katika ndoa kwa muda wa miaka mitatu tayari anakua mwanandoa halali.

Kundi hili lilitoa mapendekezo ya kutolewa kwa elimu juu ya masuala ya ndoa kabla ya watu kuingia katika ndoa na uwepo wa sheria za kuondoa ukatili na kuleta usawa katika jamii zetu. Boniphace alisisitiza kwamba uwepo wa sheria madhubuti ndio mkombozi pekee wa wanyonge kwani bila hivyo watu walio matajiri wanapendelewa.

Mshiriki Ally Thabit kutoka Mwanza alichaguliwa kutoa mrejesho wa kundi namba mbili ambao kisa mkasa chao kilimuhusu Bwana Musa ambaye alifungua akaunti tatu za siri na pia kujenga hoteli kisiri bila mkewe kufahamu, kisa hicho mwishoni kinaonyesha Bwana Musa alifariki ghafla na hivyo kuleta msuguano mkali sana katika familia yake kuhusu mgawanyo wa mali.

Huku akijibu maswali ya mirathi yaliyojitokeza katika kisa hicho Ally anataja, miongoni mwa hasara nyingine, kwamba kwanza haki ya urithi imepotea, pili usiri wa baba umekuwa kikwazo katika familia kupata haki ya msingi lakini tatu kwamba huenda wakati Bwana Musa anafariki kulikuwa na pesa nyingi katika akaunti yake benki ambazo zingeisaidia familia yake ambayo kwa mujibu wa kisa hicho hivi sasa familia hiyo inakumbwa na janga kali la umaskini.

Katika kuelezea umuhimu wa wosia; Ally aliendelea kusema kwamba wosia huondoa utata inapotokea kifo na vilevile wosia huondoa chuki na fitna baina ya ndugu na jamaa.

Mwanamke anaweza kuwa msimamizi wa mirathi
Naye Faudhia Yassin ambaye ni mratibu wa kampeni ya TUNAWEZA kutoka WLAC aliwaeleza wanakijiji kwamba Mwanamke amekuwa akitengwa sana katika ugawaji mali hivyo ni muhimu jamii kutambua kwamba hata wanawake waliofiwa na waume zao wanaweza kuwa wasimamizi halali wa mirathi.

Faudhia alisema ikitokea baba amefariki, familia ichukue cheti cha kifo na kukipeleka mahakamani kuomba mahakama imuidhinishe waliyempendekeza kuwa msimamizi wa mirathi.

Ndoa halali ni ipi?
Kundi la tatu liliwakilishwa na Mama Shujaa wa chakula Grace G.D. Mahumbuka kutoka Kagera pamoja na vijana wa Maisha Plus ambao ni Bakari Khalid kutoka Shinyanga na Said Kawawa kutoka nchini Uganda.

Kundi hili liligundua kwamba mtoto wa kike hathaminiki kama ilivyo kwa mtoto wa kiume, lakini elimu pia ya uelewa juu ya mambo ya haki ni duni. Sehemu ya kisa hicho iliwataja watu wawili wa jinsia tofauti walioishi pamoja kwa kipindi cha miaka 12 bila kuwa na ndoa hata ya kimila.

Aidha kundi hili lilipendekeza sheria ya ndoa ya Tanzania iboreshwe na kwamba ifahamike kuwa mtoto wa kike ana haki ya kurithi sehemu ya mali ya wazazi wake sawa sawa na ilivyo kwa mtoto wa kiume.

Waliendelea kwa kushauri kwamba inapotokea tatizo katika ngazi ya familia baina ya mke na mme basi aliyetendewa ukatili ajaribu kusuruhisha katika ngazi ya familia ikishindana basi aende katika ustawi wa jamii, baraza la kata, ofisi za ushauri wa kisheria za mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali kama itashindikana kote huko basi mwisho achukue hatua za kisheria za kimahakama.

Akifafanua kuhusu hoja hii, Mwanasheria Juvenile Rwegasira kutoka WLAC alisema kwamba watu wawili wa jinsia tofauti wakiishi pamoja kwa kipindi cha miaka miwili mfululizo na jamii ikafahamu kwamba hawa ni mme na mke, hiyo kisheria inaitwa dhana ya ndoa.

Mwanasheria Rwegasira alisisitiza kwamba ni lazima iwe miaka miwili mfululizo na sio ile ya kuja miezi miwili na kuondoka na kuja tena na kuondoka.

Hata hivyo, Bw. Rwegasira alitoa angalizo kwamba ndoa hii ni rahisi sana kukanushika hivyo akasisitiza umuhimu wa kuhitaji tamko la Mahakama kuidhinisha dhana ya ndoa.

Akiendelea Bw. Rwegasira alisema kwamba ndoa hii ni ya kienyeji mno na haina cheti hivyo ikitokea mmoja amefariki inaleta shida sana kwenye ugawaji wa mali.

Pata msaada wa kisheria BURE
WLAC ni kituo cha msaada wa kisheria kwa wanawake. Kwa wenye matatizo ya Mirathi, Ndoa, Ardhi, Elimu, Ajira, Matunzo ya Watoto na Mengineyo wapige simu BURE kwenda namba 0800780100

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni